"naomba" poems
Taifa haliwezi kuwa na maendeleo ikosekanapo hekima,
Nchi haiwezi kuwa na chakula pasipo wakulima,
Jamii haiwezi pata maendeleo pasipo kujituma,
Siasa yetu leo ni ya kuwasha na kuzima,
Maneno yasemwayo hayaingii akilini mwa mtu mzima,
Madaraka wanajipatia na vyeo kwa lazima,
Hawajali ya jana wala leo wanajali shibe yao,
Wanalimbikiza mali kwa miradi ya wanao,
Wanaikandamiza haki kwa kutumia elimu yao,
Demokrasia imekuwa kinga yao dhidi ya ufisadi wao,
Siasa imekuwa nyimbo tena zile za mwambao,
Wakisemana kwa mafumbo wanajuana wao,
Wanakaa majukwaani na makubwa yao matumbo,
Mzee alisema fumbo mfumbie mjinga,
Busara na hekima ni kumsikiliza anaye kupinga,
Maana hoja zake zawezekana zikawa za kujenga,
Utajuaje siri ya adui yako bila kumpenda,
Kamwe huwezi kushinda mechi kwa kujua kupiga chenga,
Kamwe huwezi kuwa na nguvu kwa kujitenga,
Naomba tukazane nchi yetu kuijenga,
Tukipamba na maadui maradhi umasikini na ujinga,
Sio kuyasifia mema ili madhaifu kuyapamba,
Ila ukweli kuusema bali tukitumia hekima,
Ikosekanapo kamba huwezi teka maji yakisima,
Ikosekanapo nanga huzamisha meli nzima,
Kuwa na vingi si kuishi kwa kujinyima,
Unapojenga msingi katu huwezi kurudi nyuma,
Mkulima mzuri hutegemea mbivu kuzichuma,
Yule aliye mvivu kamwe hawezi kujituma,
Daima yeye aliye msikivu hujifunza na kuelewa,
Ila Yule aliye mvivu hutegemea ngekewa,
Wanasiasa hulalamika kana kwaamba wanaonewa,
Ukweli ni kwamba wanatumia vibaya uhuru waliopewa,
Daima taifa haliwezi endelea ikosekanapo hekima.
© issai
Jun 26, 2014
Jun 26, 2014 at 6:04 AM UTC